KIUNGO Uhuru Suleiman Mwambungu ameongeza mkataba
wake kwa miaka miwili na klabu yake, Simba SC na kufuta taarifa zilizomhusisha
na Yanga waliokuwa wanamtaka mchezaji huyo.
Uhuru aliwasili Simba
misimu miwili iliyopita akitokea Mtibwa Sugar ya Morogoro, iliyomtoa Coastal
Union ya Tanga amesema kwamba ameongeza mkataba wa miaka miwili na klabu yake.
“Kaka nimesaini
mkataba mpya wa miaka miwili na hivi ninavyozungumza na wewe nimekuja kwetu
Mbeya kijijini kabisa kuchukua baraka za wazee, kisha nirudi kazini na nguvu
mpya,”alisema Uhuru.
Uhuru hakutaka
kuwazungumzia Yanga, kwa sababu amesema hakuwahi hata kukaa nao meza moja zaidi
ya kusikia tetesi kwamba wanamtaka.
“Nilisikia Yanga
walikuwa wananitaka, ila kwa kweli mimi naona wamechelewa, kwa sababu
nimekwishaongeza mkataba na timu yangu,”alisema.
Wachezaji wengine wa
kikosi cha kwanza Simba msimu huu, ambao mikataba yao imeisha ni mabeki Juma
Nyosso na Juma Jabu, ambao nao wanahusishwa na mpango wa kuhamia kwa mahasimu
wa jadi, Yanga.






