MWENYEKITI wa klabu ya Yanga, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga
ametangaza kujiuzulu wadhifa wake ofisini kwake, jengo la NSSF, barabara ya
Bibi Biti, Dar es Salaam, baada ya kuvamiwa na kundi la watu nyumbani kwake,
Mbezi, Jijini usiku wa wa manane.
Lakini Nchunga amekataa kulihusisha tukio hilo na kujiuzulu kwake,
akisema kwamba amefikia uamuzi huo ili kuinusuru Yanga, kwa sababu wapo watu ambao
wako tayari Yanga ife, lakini wamng'oe yeye madarakani, kitu ambacho yeye
hataki kitokee.
Nchunga alisema kuwa majira ya saa nane usiku, alivamiwa na kundi la
watu takribani 15, lakini hawakufanikiwa kufanya chochote kutokana na ulinzi
mkali uliopo katika nnyumba hiyo.
"Kwanza mbwa walianza kubweka, walinzi wakashituka wakaomba
msaada kwa walinzi wenzao, nasi tukapuga simu polisi, wakaja haraka sana na
kukuta watu hao wamekwishakimbia,"alisema
TAARIFA YA KUJIUZULU KWA NCHUNGA:
LLOYD NCHUNGA BIHARAGU
C/O LLOYD ADVOCATES,
Morogoro/Bibi TIti Mohamed
Rd,7th Floor, J.K. Nyerere Pension towers
P.BOX 75111, Dar-Es- Salaam,Tanzania.
TAARIFA KWA
VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KUJIUZULU NAFASI YA UENYEKITI WA KLABU YA YANGA.
Ndugu wana Habari, najua kwamba taarifa hii itawafedhehesha wajumbe
na wanayanga wanaotuunga mkono,hasa ukizingatia maamuzi ya pamoja ya vikao
vyetu vya kamati ya utendaji vilivyopita kwamba hakuna wa kujiuzulu kati yetu
mpaka tujue hatma ya mkutano mkuu ambao tulipanga ufanyike tarehe 15 Julai 2012,
ukiachia mbali shinikizo la kujiuzulu linalotolewa na baadhi ya wazee na
wanaojiita vijana wa klabu, kwa wajumbe wa kamati ya utendaji, na hasa mimi
kama mwenyekiti.
Nawashukuru wajumbe kwamba tulifanya kazi kwa pamoja na kwa
ushirikiano mzuri, na hata pale tulipotofautiana tulifanya hivyo kwa hoja na
kufikia maazimio ambayo wote tulikuwa tunawajibika nayo.
Tangu tumeingia madarakani tumeweza kushirikiana na kupata mataji
matatu katika kipindi cha mwaka mmoja, yaani; Ngao ya Hisani 2010, Ubingwa wa
ligi kuu ya Vodacom 2010/2011, na Ubingwa wa
Afrika Mashariki na Kati (Kagame Cup), 2011. Zaidi ni kwamba tulifuta
uteja kwa watani wetu wa jadi kila tulipokutana katika ligi ukiachia mbali
mechi ya tarehe 6 Mei 2012, ambayo tulifungwa goli 5 bila, na kuleta mtafaruku
mkubwa katika klabu yetu.
Hali kadhalika tumeshirikiana
mpaka tumeweza kuboresha mkataba kati yetu na TBL kupitia Kilimanjaro
Premium Lager, tumeingia mkataba na
kampuni ya NEDCO kuendeleza mali
zetu katika mtaa wa mafia na uwanja wetu wa KAUNDA baada ya kufikia hatua nzuri
katika kupata hati miliki za maeneo yote mawili. Nafahamu kwamba kampuni hiyo
iko katika hatua za mwisho za kumalizia michoro.
Hali kadhalika tuliingia mkataba wa kuzalisha na kuuza bidhaa zenye
nembo yetu na hasa baada ya kufanya marekebisho yatokanayo na matakwa ya sheria
kule BRELA na pia mkataba na kampuni ya NEXUS LTD, ambayo itakuwa inatutafutia
wadhamini wa nje na ndani, kufanya promosheni zetu na kampeni kwa njia ya
electronic kupitia mitandao mbalimbali na kukusanya data za wanachama na
kusajili wapya tukiwa na malengo ya
kukusanya shilingi 300,000,000/= hadi 800,000,000/= kwa mwaka katika kipindi
cha miaka mitatu. Haya yote tuliyafanya tukilenga kujitegemea kujazia mapengo
yaliyokuwa yakitokana na kutegemea ufadhili wa mtu mmoja mmoja.
Kwa ridhaa yenu tumekua tukiendelea na mazungumzo na makampuni mbali
mbali kwa ajili ya udhamini na kwa sababu maalum, nitazitaja katika hati ya
makabidhiano kwa kiongozi ajaye.
Aidha, tumeshirikiana katika kufanya mambo mbali mbali ya kijamii,
ikiwa ni pamoja na sikukuu ya kuadhimisha miaka 77 ya Yanga, sikukuu za pasaka,
kuchangia jamii na waliokumbwa na maafa, na kongamano la vijana lililolenga
kuwaamsha vijana kuitambua nafasi yao katika Yanga ikiwa ni pamoja na kupata
azimio la kuanzisha SACCOSS ya Yanga, ambapo maombi yapo kwa msajili Manispaa
ya Ilala.
Haya yote nayataja ikiwa ni kuwashukuru kwa ushirikiano na
ikiwezekana muweze kuyakamilisha yaliyobaki ambayo mtaona yalikuwa mazuri.
Lakini pia tulipopata matatizo tulikuwa pamoja. Nichelee kusema tu kwamba tulisimama pamoja
baada ya kujiuzulu Makamu Mwenyekiti wetu Ndugu Davis Mosha na mjumbe wetu ndugu Seif A. Seif, Ali Mayayi, na wengineo,
kwani tulifungwa na katiba.Tulisimama pamoja pia katika suala la kujiuzulu
ndugu Yusuf M. Manji, aliyekuwa mdhamini mteule na mfadhili mkuu ambaye sasa
ameonyesha nia ya kurudi nanyi mkaridhia mkutane naye. Awali, tulitumia kila
jitihada za kumrejesha lakini ikashindikana.
Hata hivyo doa limetupata baada ya kufungwa na watani wetu goli 5
bila, ambapo kuna wanachama wanaoelewa na wasioelewa kabisa.
Ninachokiona mimi ni usaliti wa hali ya juu uliombatana na matukio
mbalimbali yaliyopita na yanayoendelea hadi kujaribu kupindua uongozi wa halali
wa kidemokrasia. SIWATUHUMU WACHEZAJI MOJA KWA MOJA, isipokuwa mfululizo wa matukio wiki tatu kabla ya
mchezo ule na sasa, inaonyesha kwamba kulikuwa na usaliti mkubwa ambao sisi
hatukuweza kuubaini mapema.
Sioni mantiki katika hoja kwamba wachezaji walikuwa wakidai
mishahara, posho n.k. Au ati mtendaji
wetu alishikiliwa Arusha kwa deni la hoteli, ndiyo tuvune bao 5!
Kwa wanaoijua Yanga, imewahi kuwa na madeni makubwa katika Hoteli
mbali mbali, mawakala wa ndege n.k, na baadhi tumeyakuta na sisi tumekuja
tukayalipa. Hii imewahi kutokea kabla na wakati akiwepo mfadhili, sembuse sisi
tulioachwa baki, na bado wachezaji walicheza kwa morali.
Hata hivyo, utamaduni wa kutimuana baada ya matokeo mabaya ni dhambi
ambayo itatula kama hatutaiacha, kwani wenye hila na uchu wa madaraka
wataendelea kutumia mbinu hiyo ili kuuondoa uongozi wa kidemokrasia.
Baada ya mapinduzi kushindikana na TFF kuonya kuhusu mapinduzi hayo,
wazee kupitia msemaji wao , Mzee Akilimali wamesikika katika kipindi cha
Michezo cha Redio moja maarufu hapa
nchini wakidai kwamba ni bora Yanga ishushwe daraja au kufungiwa kuliko mimi
kuendelea kuongoza!
Hii imenikumbusha HEKMA ZA MFALME SELEMANI akiamulia ugomvi wa
wanawake wawili waliokuwa wakigombea mtoto naye akaamuru wamgawane nusu kwa
nusu. Yule mwenye mtoto kweli alimuomba Mfalme amuachie mwenzie kuliko kumkata
nusu.
Kwa hekma hiyo nimeamua kujiuzulu nafasi yangu katika Uenyekiti wa Yanga kwani ni klab ninayoipenda hata kama
sio kiongozi kwa mujibu wa ibara ya 28 ya katiba yetu.
Vile vile siko tayari kuona klab yangu ikisalitiwa au kuhujumiwa eti
kwa sababu tu mimi ni kiongozi.
Natumaini kamati ya utendaji kwa pamoja na wale tuliowateua chini ya
ibara ya 29(3) ya katiba ya Yanga pamoja na bodi ya wadhamini, itawaongoza
wanachama mpaka kufikia mkutano mkuu kwa
mafanikio zaidi.
Nitaendelea kuwa mwanachama
mwadilifu na nitatoa mchango wangu wa hali na mali pale nitakapo hitajika na
nikiwa na uwezo wa kufanya hivyo.
YANGA DAIMA MBELE, NYUMA MWIKO.
Wasalaam,
LLOYD NCHUNGA BIHARAGU.
Nakala kwa:-
Mama Fatma Karume,Mdhamini
Francis Kifukwe, Mdhamini
Bwana Yusuf Manji – Kwa taarifa