Timu ya soka ya taifa
ya Tanzania, Taifa Stars imeanza kujifua ikiwa Ivory Coast kujiandaa na mechi
ijayo ya kuwania kufuzu fainali za kombe la dunia 2014 nchini Brazil, dhidi ya
Gambia itakayochezwa Jumapili ijayo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kocha Mdenmark, Kim
Poulsen, leo aliiongoza Taifa Stars kufanya mazoezi asubuhi kwenye uwanja wa
Shirikisho la Soka la Ivory Coast (FIF) pembezoni mwa jiji la Abidjan.
Timu hiyo itafanya
tena mazoezi kesho (Juni 4 mwaka huu) asubuhi kabla ya kuanza safari ya kurejea
nyumbani saa 1.30 usiku kwa ndege ya Kenya Airways kupitia Nairobi ambapo
itawasili Dar es Salaam, Juni 5 mwaka huu saa 1.40 asubuhi.
Kocha Kim aliwakosa
wacheaji wanne ambao ni majeruhi (Thomas Ulimwengu, Nurdin Bakari, Haruna Moshi
na Nassoro Masoud Cholo) amesema hivi sasa wameelekeza mawazo yao kwenye mechi
ijayo dhidi ya Gambia.
“Safari ya kujenga
timu ndiyo imeanza. Mechi dhidi ya Ivory Coast imepita na ninawashukuru
wachezaji kwa kucheza kwa mujibu wa maelekezo na kujituma. Mpira ni mchezo wa
makosa, tumefanya makosa yaliyosababisha tuwape Ivory Coast mabao mepesi.
“Lakini kama
nilivyosema mechi hiyo imepita, hivi sasa tunaangalia mechi ijayo dhidi ya
Gambia. Hatuna muda mwingine wa kujipanga na ndio maana niliamua kuja na
wachezaji wote Abidjan,” amesema Kim.
Mechi dhidi ya Gambia
itachezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 jioni. Gambia ilitoka
sare ya bao 1-1 na Morocco katika mechi iliyochezwa juzi jijini Banjul.
Taifa Stars itamkosa
na nahodha msaidizi, Aggrey Morris aliyeoneshwa kadi nyekundu dakika ya 65
baada ya kupata ya pili ya njano kwenye mechi dhidi ya Ivory Coast iliyochezwa
Uwanja wa Felix Houphouet-Boigny jijini Abidjan.
No comments:
Post a Comment