RAIS mstaafu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya awamu ya pili, Alhaji Ally Hassan Mwinyi, amechaguliwa kuwa
mgeni rasmi katika sherehe za utoaji tuzo za wanamichezo bora Tanzania zitakazofanyika hapo kesho
kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Chama
cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), Juma Abbas Pinto amesema hayo
kwenye Mkutano na Waandishi wa Habari mchana huu katika ukumbi wa City Sports
Lounge, jijini Dar es Salaam na kwamba wamemchangua Mwinyi kwa sababu alikuwa ana
mchango mkubwa katika sekta ya michezo enzi zake, akiwa Ikulu tangu 1985 hadi
1995 alipomuachia Benjamin William Mkapa.
Katika tuzo hizo,
kiungo wa kimataifa wa Rwanda, Haruna Fadhil Hakizimana Niyonzima wa Yanga,
atachuana na Kipre Tchetche wa Ivory Coast anayechezea Azam FC na Mganda
Emmanuel Okwi wa Simba kuwania tuzo ya Mwanasoka Bora wa mwaka wa kigeni.
Kwa upande wa wanasoka
wazalendo, tuzo ya Mwanasoka Bora wa Mwaka inawaniwa na John Bocco, Aggrey
Morris, wote wa Azam na Juma Kaseja wa Simba, wakati kwa wachezaji wa Tanzania
wanaocheza nje wanaoshindana ni Henry Joseph wa Kongsvinger ya Norway na Mbwana
Samatta wa Tout Puissant Mazembe ya DRC.
Kwa upande wa
wanawake, Sophia Mwasikili anayecheza Uturuki, anashindana na Asha Rashid
‘Mwalala’, Mwanahamisi Omary wote wa Mburahati Queens, Fatuma Mustapha wa
Sayari na Eto’o Mlenzi wa JKT.
Tuzo hizo zinadhaminiwa
na Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL).

No comments:
Post a Comment