VIEW OTHER SITES

Wednesday

MBELGIJI WA YANGA KUTUA LEO


Kocha mpya wa Yanga, Thom Saintfiet, kutoka Ubelgiji anatarajiwa kuwasili leo Dar es Salaam, tayari kuanza kazi ya kukinoa kikosi cha mabingwa hao wa Afrika Mashariki na Kati, Kombe la Kagame.
Ofisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu alisema jana kwamba, Thom aliyekuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa Shirikisho la Soka Nigeria, akiwasili atakwenda moja kwa moja kufanya mazungumzo na uongozi kwa ajili ya kusaini mkataba.
Alisema Saintfiet ataanza kazi mara moja atakapowasili na kumaliza kusaini mkataba, ili kuiandaa timu kwa ajili ya kutetea Kombe la Kagame, michuano inayotarajiwa kuanza Julai 14, mwaka huu, Yanga ikifungua dimba na mabingwa wa Burundi, Atletico.
Mbelgiji huyo anakuja kurithi mikoba ya Mserbia, Kostadin Bozidar Papic aliyetupiwa virago mwishoni mwa msimu.
Tangu kutupiwa virago kwa Papic zikiwa zimesalia mechi tatu ligi kumalizika, Yanga imekuwa chini ya Kocha wake Msaidizi, Freddy Felix Minziro.
Ujio wa Mbelgiji huyo, unamaliza zama za makocha wa Kiserbia waliokuwa wakibadilishana uongozi wa benchi la ufundi la Yanga, tangu mwaka 2007, kuanzia Milutin Sredojevic ‘Micho’ aliyewaachia Profesa Dusan Savo Kondic, Spaso Sokolovoski na Serdan Civojnov, ambao nao walimuachia Papic.
Awali, Papic alipoondoka nafasi yake ilichukuliwa na Mganda, Sam Timbe aliyeleta mataji mawili, ubingwa wa Ligi Kuu na Kombe la Kagame, lakini akarudishwa tena Mserbia huyo msimu uliopita kabla ya kutupiwa virago mwishoni mwa msimu.

No comments:

Post a Comment