Pambano la Ligi Kuu ya Vodacom (VPL)
kati ya wenyeji Azam na Yanga lililochezwa jana Septemba 22
katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam limeingiza sh. 138,188,000.
Watazamaji waliokata tiketi kushuhudia
pambano hilo namba 33 la VPL msimu wa 2013/2014 lililomalizika kwa Azam
kuibuka na ushindi wa mabao 3-2 walikuwa 24,020.
Viingilio katika mechi hiyo vilikuwa sh.
5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata
mgawo wa sh. 33,065,409.1 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT)
iliyolipwa ni sh. 21,079,525.42.
Mgawo mwingine wa mapato hayo ni
asilimia 15 ya uwanja sh. 16,812,919.89, tiketi sh. 5,022,342, gharama
za mechi sh. 10,087,751.93, Kamati ya Ligi sh. 10,087,751.93, Mfuko wa
Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 5,043,875.97 na Chama cha Mpira wa
Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 3,923,014.64.
Mechi iliyopita ya VPL kwenye uwanja huo kati ya Simba na Mbeya City iliingiza sh. 123,971,000.
MECHI YA TOTO, POLISI DOM KUPIGWA J2
Mechi namba 12 ya Ligi Daraja la Kwanza
(FDL) kati ya Toto Africans na Polisi Dodoma iliyokuwa ichezwe Jumamosi
(Septemba 28 mwaka huu) Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza imesogezwa
mbele kwa siku moja.
Timu hizo za kundi C sasa zitapambana
Jumapili (Septemba 29 mwaka huu) kwenye uwanja huo huo ili kupisha mechi
namba 10 kati ya Pamba na Stand United FC ya Shinyanga itakayochezwa
Jumamosi (Septemba 28 mwaka huu).
Mechi nyingine za kundi hilo
zitakazochezwa Jumamosi ni Mwadui na Polisi Tabora (Uwanja wa Kambarage,
Shinyanga) wakati Kanembwa JKT na Polisi Mara zitacheza kwenye Uwanja
wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)